Wednesday 13 July 2011

Njama Inaiva


Ndipo basi Sungura akamwandama Swara. Alimpata Swara kajitambaza kuota jua mikono kama ambaye yuapiga dua. Swara alikuwa bado hajamwona Sungura na kwa ujanja wake Sungura alipapasa Swara mkiani kwa makucha yake madogo. Kwa mshtuko mkubwa Swara aliruka juu akatoka mbio kisi cha mita hamsini kasha akaangalia nyuma. Sungura kwa wakati ule alikuwa ameangua kicheko, mbavu zauma.

“Nakuonya kabisa Sungura ukome mzaha kama huo” Swara akamwambia Sungura. “umenifanya nikadhani mmoja wa majemedari amenishika akapata chakula cha mchana na mabaki ya kumpelekea mfalme. Naye Sungura akamajibu akisema hakufikiri Swara ni mwoga kiasi hicho. “Nitakosaje kuwa mwoga huku wenzangu wakiliwa kila siku na hawa kina Simba na majemedari wake” Swara akamuuliza. Naye Sungura akamjibu “Nikidhani ni sisi tu akina Sungura tulio na shida. Ninyi mnayo bahati pamoja na familia ya kina Ndovu na Rhino kwani mataifa ya nje hasa nchi ya binadamu wanawatetea msije mkamalizwa kwenye sura ya dunia”.  

“Nimesikia jambo kama hilo kweli, lakini walio na bahati sana ni kina ndovu kwani kuna kamati kubwa sana wa binadamu wote wanawatetea ndovu wasuawe kwa sababu ya pembe zao” akasema Swara. Hapo Sungura akapata nafasi ya kuelezea kilicho moyoni mwake. “Kwa maoni yangu ikifanywa sensa ya wanyama pori wote, sisi ambao hula nyasi na mimea ndio wengi kuliko wale walao nyama au sio”. Sungura akamjibu kwa kukubaliana naye. “Linalosikitisha ni kwamba sisi tulio wengi tumekubali kutawalwa ki mabavu na hawa walowezi walao nyama na kunywa damu kama vile Simba na….” Kabla hajamaliza aliyotaka kuyasema, Swara akamkatiza “Jambo hilo hunisumbua na kunikera mno kwani hatuachwi kuishi kwa amani yetu, kula bila hofu ya hao majemedari wa mfalme”. Sungura akamjibu “mimi naona tuungane wanyama wote tuipindue huu utawala wa Simba. Swara naye akafurahishwa na wazo hilo lakini akawa hajui waanze wapi. Huku akiwa na mchanganyiko wa mawazo akamkumbusha Sungura mambo machache kuhusu huyo mfalme “Kaka yangu Sungura kumbuka nguvu za mwili lilo nazo hilo jinyama. Mkono, paja na makucha yake. Mdomo kubwa waweza toshea wewe na dadako mmzo mmoja, na meno yalio na makali kama msumeno”. Sungura naye akasisitiza wasiuogope mwili mnene wa Simba “Simba ana miguu miwili na mikono miwili kama tulivyo sisi. Anachotuzidi nacho ni mwili mkubwa lakini kiakili hatushindi kabisa. Sisi japo tuna mwili mdogo, tunao ujanja na werevu mwingi kumshinda huyo mfalme”. Swara akakubaliana naye lakini akazua hoja kwamba haiwezekani kwao wakiwa wawili kumng’atua Simba madarakani bila ushirikiano wa wanyama wote walao mimea.

No comments:

Post a Comment